Saturday, 24 January 2015

Wananchi waapisha viongozi - Tabata Segerea
Na Stephen kitomary
VIONGOZI wa serikali ya mtaa wa Migombani, kata ya Segerea, wilaya ya Ilala, wameapishwa na wananchi. MwanaHALISIonline linaandika.
Kiapo hicho kimefanyika leo, baada ya Halmashauri ya Manispaa ya Ilala kushidwa kutimiza wajibu wake kwa muda uliopagwa kwa mujibu wa sheria na kanuni za uchaguzi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji za mwaka 2014.
Wakizungumza na MwanaHALISIonline, wakazi wa mtaa huo wamesema, kutoapishwa kwa viongozi wa waliowachagua kumeathiri masuala ya maendeleo katika eneo hilo, hali iliyopelekea kuchukua uamuzi wa kumuita wakili anayetambulika kisheria kuwaapisha viongozi wapya.
“Wananchi wamechoka. Wameamua kubadilisha uongozi kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM) na kukiweka Chama cha Demokrasi na maendeleo cha Chadema Madarakani ….
“Lakini tayari zimepita siku 30 bila viongozi kuapishwa. Mkurugenzi wa Halmashauri, Issaya Mungurumi, haijatoa sababu ya msingi ya kushidwa kuwaapisha viongozi. Tumeamua kuchukua jukumu hilo sisi wenyewe kwa sababu ndiyo tunaopata shida,” amesema Obedi John, mkazi wa mtaa huo.
Akizungumza na MwanaHALISIonline baada ya kuapishwa, Mwenyekiti wa Mtaa huo Japhet Albert Kembo amesema “wananchi wamechoka kukaa bila huduma za serikali ya mtaa, leo saa 2:30 asubuhi wamekuja nyumbani kwangu na kunitaka  niende ofisi ya serikali ya mtaa nikaapishwe”
Kiapo hicho kimefanyika nje ya ofsi ya serikali ya mtaa chini ya Wakili wa kujitegemea Iddi Msawangu, huku ofisi zikiwa zimefugwa na Afisa mtendaji wa mtaa, Suzan Zephania akitoweka kusiko julikana dakika 20 kabla ya tukio hilo kuanza.
Msawangu amesema “Leo nimewaapisha viongopzi wa serikali ya mtaa akiwemo mwenyekiti, wajumbe watatu wa kamati ya mtaa waliohudhuria, huku wajumbe wengine wakiomba udhuru.”
Aidha, Msawangu amesema amefanya kazi hiyo baada ya kuobwa na wananchi ikiwa ni sehemu ya kutimiza majukumu yake kwa mujibu wa sheria.
Issaya Mungurumi, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, alipotafutwa kwa njia ya simu na MwanaHALISIonline, kuzungumzia tukio hilo amejibu kwa kifupi “ Sina taarifa kuhusu viongozi kuapishwa na wananchi. Zipo sababu za msingi za kucheleweshwa kwa zoezi hilo kwa mitaa mitatu. Ukinitafuta ofsini kwangu, nitakueleza kwa undani. Tunatarajia kuwaapisha viongozi ndani ya wiki hii”
Mungurumi alipoulizwa ni sababu zipi zilizochelewesha uapishwaji amesema “ Kwa sasa siwezi kuongea. Nipo Kwenye kikao nitafute wakati mwingine.”
Samweli Binagi, aliyekuwa Mwenyekiti wa mtaa huo kwa tiketi ya CCM amesema “kama wananchi wameamua kuchukua hatua hiyo ambayo haina tatizo la kisheria mimi sina tatizo na umauzi waliouchukuwa wa kuwaapisha viongozi waliowachagua.”

Mtaa wa Migombani, anakoishi Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Didas Masuburi ulifanya uchaguzi wa nafasi ya Mwenyekiti wa mtaa 14 Desema, 2014 huku Mgombea wa Chadema Japhet Albert Kembo akishinda kwa kura 547 kati ya kura 1057 zilizopigwa huku idadi ya waliojiandikisha ikiwa ni 1565.
Nafasi ya pili ilichukuliwa na mgombea wa CCM, Uyeka Lumbyambya alipata kura 273 huku nafasi ya tatu ikichukuliwa na mgombea wa NCCR Mageuzi Elick Mchata aliyepata kura 205.
Aidha, uchaguzi wa wajumbe wa kamati ya mtaa ulifanyika 21 Desemba, 2014 na Chadema kushinda viti vyote.
mwisho












No comments:

Post a Comment